Chuo cha Ustawi wa Jamii

wanawake ISW washiriki kilele cha siku wa kimataifa ya wanawake mkoa wa dar es Salaam

Watumishi Wanawake wa Chuo cha Ustawi wa Jamii wameshiriki kikamilifu katika maadhimisho ya kilele cha siku ya kimataifa ya wanawake tarehe 8 Machi, 2026, ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mh. John Chalamila katika viwanja vya Barafu Mburahati, mkoani Dar es Salaam.

WANAWAKE ISW WAWAGUSA KWA ZAWADI WAGONJWA ZAHANATI YA KIJITONYAMA

Kuelekea kilele cha Siku ya Mwanamke Duniani, Wanawake wa Chuo cha Ustawi wa Jamii, tarehe 6 Machi 2026, wakiongozwa na Naibu Mkuu wa Chuo Utawala Dkt. Zena Mabeyo wametembelea na kutoa zawadi mbalimbali Zahanati ya Kijitonyama zitakazosaidia kuboresha huduma katika Wodi ya Wazazi. Akizungumza baada ya kupokea zawadi hizo Mganga Mfawidhi wa Zahanati hiyo, Dkt. Faraja Mgana amesema ni heshima na upendo mkubwa ambao wanawake wa ISW wameonyesha kwa wagonjwa wanaopata matibabu kwenye zahanati hiyo, lakini zaidi tendo hili limedumisha mahusiano mazuri na ujirani mwema kati ya Chuo cha Ustawi wa Jamii na Zahanati ya Kijitonyama.

Dkt.Joyce: Familia imara msingi wa taifa lenye ustawi

Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii, Dkt. Joyce Nyoni Mkuu amesema familia ni taasisi ya kwanza ya kijamii ambayo binadamu huikuta kabla ya shule, kanisa au msikiti na ajira. Aidha,amesema ndani ya familia ndipo mtoto hujifunza lugha, maadili, heshima pamoja na kujifunza namna ya kuishi na wengine. "Tunaposema familia yangu, Taifa langu” tunamaanisha kuwa ubora wa Taifa ni kioo cha ubora wa familia zake,"alisisitiza. Dkt.Joyce ameyasema hayo leo Machi 6,2026 wakati akiwasilisha mada kuhusu familia yangu Taifa langu katika Kongamano la Wanawake 2026 lililoandaliwa na Shirika la Utangazaji (TBC) kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake duniani katika Ukumbi wa Mkataba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mgeni rasmi katika kongamano hilo alikuwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia ,Wanawake na Makundi Maalum, Mh. Dkt.Dorothy Gwajima. "Ikiwa familia zetu zina amani, Taifa litakuwa na amani Ikiwa familia zetu zina misingi ya haki, Taifa litakuwa na misingi ya haki,ikiwa familia zetu zina usawa, Taifa litakuwa jumuishi,"amesisitiza. Aidha,amesema kuwa amani ya Taifa huanzia kwenye amani ya familia na kwamba familia yenye migogoro, dhuluma na ukatili huathiri afya ya akili ya watoto. "Watoto wanaokulia katika mazingira ya vurugu wana uwezekano mkubwa wa kuendeleza vurugu, kukosa utulivu wa kisaikolojia, kushindwa kufikia uwezo wao wa juu,"amesema ambaye kitaalum ni Daktari wa Sosholojia.

Mh. Naibu Waziri Mhandisi MaryPrisca Mahundi Ajionea Wataalamu wa ECCD wanavyoandaliwa ISW Kisangara

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mha. MaryPrisca Mahundi (MB) akiskiliza wasilisho la taarifa ya utendaji wa Chuo cha Ustawi wa Jamii Kampasi ya Kisangara, kutoka kwa Meneja wa Kampasi hiyo Dkt. Leah Mwaisango ikiwa ni sehemu ya pili ya ziara yake ya kukagua na kupata taarifa ya Shughuli mbali mbali za Chuo cha Ustawi wa Jamii. Mhe. Mha. Naibu Waziri Mahundi katika ziara hiyo aliyoifanya tarehe 25 Februari 2026, aliambatana na Uongozi wa Wilaya ya Mwanga, Kamati ya Ulinzi na Usalama na Uongozi wa Kijiji cha Mbambua Kisangara, Mwanga.

Wanafunzi Chuo cha Ustawi wa Jamii wakusanya vikombe SHIMIVUTA Tabora

Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii Dkt. Joyce Nyoni amepokea ujumbe wa wanafunzi walioshiriki mashindano ya #Shimivuta yaliyofanyika mkoani Tabora kuanzia tarehe 11 hadi 23 Desemba 2025. Katika michuano hiyo timu za wanafunzi wa #ISW zimetwaa vikombe, medali na vyeti vya ushindi kama ifuatavyo; medali ya mshindi wa pili mbio za mita 400 wanawake, kombe la mshindi wa tatu karata, kombe la mshindi wa kwanza mbio za magunia na cheti cha timu yenye nidhamu bora mshindi wa pili. "Ni heshima kubwa kwa chuo kwa ushindi huu mlioupata, ushindi huu uwe mfano na kipimo cha juhudi za kufanya vyema zaidi mashindano yajayo," alisema Dkt. Joyce. Kwa mujibu wa mkuu wa chuo, ameeleza kuwa michezo ni nyenzo muhimu ya kuwafanya wanafunzi kuwa imara na shupavu. Aidha, aliwahimiza kuendelea na mazoezi kwa kuwa michezo huchochea ufaulu katika masomo yenu, huongeza mahusiano mema katika ya vyuo na wanafunzi wenzenu kutoka vyuo mbali mbali. Naye, Selemani Mwenda Kiongozi wa Michezo kutoka Serikali ya Wanafunzi (ISWOSO), amemuahidi Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii kuwa wataongeza ushawishi kwa wanafunzi wengi kushiriki michezo ili kuibua vipaji ambavyo baadaye huzaa ajira na kipato kwa kila mmoja ambacho huchangia maendeleo binafsi na taifa kwa ujumla

WAHITIMU CHUO CHA USTAWI WA JAMII WATAKIWA KUBADILI HUDUMA ZA USTAWI WA JAMII KUWA BIASHARA

Wahitimu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii (ISW) wametakiwa kuwa wabunifu na kubadilisha elimu ya huduma za ustawi kuwa biashara ili kujiajira wenyewe huku lengo kuu ni kutatua changamoto zilizopo ndani ya jamii zao. Akizungumza katika Mahafali ya 49 ya Chuo cha Ustawi wa Jamii Kampasi ya Dar Es Salaam na Mahafali ya nane ya Kampasi ya Kisangara kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, Mkuu wa Wilaya Temeke, Sixtus Mapunda amewaasa kuitumikia taifa kwa utii na uadilifu. "Mkawe wabunifu mkajiongeze dunia imebadilika mahitaji ya wananchi ni mengi Elimu ya saikolojia haikuwa biashara kwasasa inahitajika sana katika jamii zetu na mnapata fedha hivyo tuhamishie huduma za ustawi wa jamii kuwa biashara kuna makampuni na taasisi wanahitaji huduma hizi tuwe na juhudi na kuna matokeo ya juhudi za muda mrefu," amesisitiza Mhe. Mapunda Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wanawake na Makundi Maalum Amon Mpanju amesema wahitimu hao katika fani mbalimbali za huduma za ustawi wa jamii watatumika kuisaidia jamii kutatua changamoto zao katika kuleta Ustawi wao. Naye Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii, Dk Joyce Nyoni amesema kwa mwaka wa masomo 2025/2026 Chuo kimeanzisha programu mpya nne ikiwemo masomo na maendeleo ya ujasiriamali, utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala, kazi za jamii, watoto na vijana na mafunzo ya makuzi na malezi ya awali kwa watoto. Amesema katika mahafali hayo kuna jumla ya wahitimu 3100 kati yao 2017 ni wanawake na wanaume ni 1083 walitunukiwa tuzo zao katika fani mbalimbali za ustawi wa jamii.

ISW YAENDELEA KUNG’ARA: YAPOKEA TUZO YA NBAA KWA MARA YA NANE MFULULIZO

Naibu Mkuu wa Taasisi Mipango, Fedha na Utawala, Dkt. Zena Mnasi Mabeyo akipokea tuzo ya Uandaaji wa Hesabu kwa Viwango vya Kimataifa vya Uhasibu wa Sekta ya Umma (International Public Sector Accounting Standards (IPSAS), kundi la Vyuo vya Elimu ya Juu Tanzania. Katika tuzo hizo Chuo cha Ustawi wa Jamii kimeibuka mshindi wa tatu,ikiwa ni mara ya nane mfululizo toka mwaka 2017 #ISW inashika nafasi za juu kwenye mashindano hayo. Naibu Mkuu wa Taasisi aliambatana na Mhasibu Mkuu, Aisha Kapande Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu za Ndani kutoka Chuo cha Ustawi wa Jamii. Tuzo hizo zimetolewa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA) usiku wa tarehe 04/12/2025 katika ukumbi wa APC Bunju, jijini Dar es Salaam.

MKUTANO WA 5 WA WADAU NA WANAFUNZI WA UANAGENZI WAJADILI MWELEKEO NA MAFANIKIO YA PROGRAMU YA UANAGENZI

Mkutano wa 5 wa Wadau na Wanafunzi wa Uanagenzi kutoka Chuo cha Ustawi wa Jamii umefanyika katika Kampasi ya Dar es salaam, ukiwakutanisha wamiliki wa Taasisi mbalimbali pamoja na Wanafunzi wanaotarajia kuanza mafunzo ya vitendo kupitia programu ya uanagenzi. Mkutano huu umefanyika kuanzia tarehe 2 – 5 Desemba, 2025. Kwa mwaka huu, programu ya uanagenzi imetimiza miaka mitano tangu kuanzishwa kwake, na imeendelea kuchangia kwa kiasi kikubwa katika kuwaandaa wanafunzi kupitia uzoefu wa moja kwa moja kazini, kuimarisha ujuzi wa kiutendaji, na kupanua mtandao wao wa kitaaluma kama sehemu ya maandalizi ya kuingia kwenye soko la ajira.

ISW YAINGIA MAKUBALIANO NA ONE TANZANITE FOOTBALL ACADEMY KUBORESHA VIWANJA VYA MICHEZO

Chuo cha Ustawi wa Jamii (ISW) kimeingia makubaliano na One Tanzanite Football Academy ya kuboresha Viwanja vya michezo #ISW Makubaliano hayo yameingiwa leo tarehe 11 Novemba, 2025 kati ya Dkt. Joyce Nyoni, Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii pamoja na Bw. Agapiti Emmanuel, Mkurugenzi Mtendaji wa One Tanzanite Football Academy. Makubaliano hayo yameshuhudiwa na Timu ya Menejimenti ya #chuochaustawiwajamii na Baadhi ya maafisa kutoka One Tanzanite Football Academy.